Thursday 28 January 2016

SIMBA YAULA TENA KWA IBRAHIM HAJIBU

Na Paul chengula, DAR ES SALAAM
MPANGO unafanywa mshambuliaji wa Simba SC, Ibrahim Hajib Migomba apewe nafasi ya winga wa Azam FC, Farid Mussa kwenda kujaribiwa klabu ya FC Olimpija Ljubljana ya Slovenia.
FC Olimpija Ljubljana Desemba ilituma mwaliko wa majaribio kwa ajili ya Farid, ili akajiunge nayo katika kambi ya Hispania mapema Januari kwa majaribio ya wiki moja, lakini Azam FC ilikataa ofa hiyo.
Na sababu za Azam FC kukataa ofa hiyo ni kujitokeza wakala aliyeahidi kumpatia nafasi Farid za majaribio Farid katika klabu za Celtic FC ya Ligi Kuu ya Scotland au Athletic Bilbao ya Ligi Kuu ya Hispania.

 
Wakala huyo alifanikiwa kuishawishi Azam FC iachane na ofa ya wakala aliyekuwa anataka kumpeleka Farid FC Olimpija Ljubljana, akidai Celtic na Bilbao zinahitaji sana wachezaji aina ya Farid.
Na sasa, Hajib anaweza kwenda kufanyiwa majaribio na mabingwa hao wa Slovenia, iwapo mipango itakwenda sawa kama inavyoshughulikiwa.
Kwa sasa Hajib, mchezaji bora wa Desemba, Simba SC yuko nje kwa majeruhi baada ya kuumia wiki iliyopita katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar ya Morogoro.
Hajib, mchezaji aliyetokea katika kikosi cha vijana cha Simba SC kabla ya kutolewa kwa mkopo Mwadui FC akapate uzoefu, alirejea Msimbazi msimu uliopita na mara moja amekuwa tegemeo la timu.

No comments:

Post a Comment