Thursday 13 August 2015

TP MAZEMBE SAFARI YA DARESALAAM,AL HILAL WASHTUKIA.

TP Mazembe wakifanya mazoezi usiku jana mjini Lubumbashi
MABINGWA mara nne Afrika, Tout Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wamesitisha mpango wa kuja Dar es Salaam kuweka kambi fupi kwa ajili ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Timu hiyo yenye Watanzania wawili, Mbwana Ally Samatta na Thomas Emmanuel Ulimwengu ilitaka kuja Dar es Salaam wiki hii kwa maandalizi ya mchezo mgumu wa ugenini dhidi ya Al Hilal nchini Sudan Jumapili ya Agosti 23, lakini imeghairi.
Habari za ndani zinasema kwamba Mazembe ilitaka kuja kwa siri Dar es Salaam, lakini baada ya habari za ujio wao kuvuja, wameamua kughairi kwa kuhofia hujuma za wapinzani wao.
TP Mazembe wakifanya mazoezi usiku jana mjini Lubumbashi

Mtendaji Mkuu wa Azam FC, Saad Kawemba aliithibitishia CHENGULA NEWS- ONLINE wiki iliyopita juu ya ujio wa Mazembe ambao waliomba kutumia Uwanja wa Azam FC kwa mazoezi.
“Wanataka kuja kutumia vifaa vyetu kwa maandalizi kwa maana ya Uwanja wa mazoezi na vitu vingine ikiwemo gym. Kimsingi tumewakubalia na kuna uwezekano pia tukacheza nao mchezo wa kirafiki,”alisema Kawemba.
Ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Smouha ya Misri wiki iliyopita mjini Lubumbashi uliipandisha kileleni mwa Kundi A Mazembe Ligi ya Mabingwa Afrika.
Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Mazembe, bao pekee la TPM lilifungwa na Roger Assale dakika ya 53 na sasa mabingwa hao mara nne Afrika wakatimiza pointi nane baada ya kushinda mechi mbili na sare mbili.
Al Hilal inabaki na pointi zake tano baada ya juzi kufungwa 1-0 nyumbani na Moghreb Tetouan ya Morocco ambayo sasa nayo imefikisha pointi tano. Smouha ya Misri ina pointi tatu. 
Na TPM imekuwa ikifanya mazoezi usiku tangu juzi katika Uwanja wake wa Mazembe kwa kuwa mechi yao na Hilal pia itachezwa usiku. Ikumbukwe mechi ya kwanza timu hizo zilitoka sare ya bila kufungana Lubumbashi.

No comments:

Post a Comment