Tuesday 20 June 2017

MKUDE AFUNGUKA YA MOYONI

KIUNGO Jonas Gerald Mkude amesema anafurahia maisha Mtaa wa Msimbazi ndiyo maana ameongeza mkataba wa miaka miwili kuendelea kuichezea Simba SC.
Akizungumza na CHENGULA NEWS, Mkude amesema kwamba anashukuru baada ya vikao mfululizo na uongozi wa Simba wamefanikiwa kufikia maafikiano, ambayo ni kuongeza mkataba wa miaka miwili.
“Ninashukuru baada ya vikao vikao na viongozi tumefanikiwa kufikia makubaliano mazuri. Nataka niwape habari nzuri wana Simba, nitaendelea kuwa nao kwa miaka mingine miwili,”amesema Mkude.

Nahodha huyo wa Wekundu wa Msimbazi, amesema kwamba kuongeza mkataba Simba ni changamoto nyingine kwake, kwani anatakiwa kuendelea kudhihirisha ubora wake Msimbazi na kuisaidia timu.
Amesifu jitihada za uongozi kuboresha kikosi kwa kusajili wachezaji wazoefu na kuwapa mikataba mipya wachezaji waliopo ambao ama wanamaliza au wanakaribia kumaliza.
“Unapotaka kujenga timu kwanza lazima uwalinde wachezaji wako wazuri ulionao, na pili usajili wapya wanaohitajika kuja kuimarisha kikosi, ndiyo maana ninawapongeza viongozi,”amesema. 
Mkude aliibukia kikosi cha pili cha Simba mwaka 2011 kabla ya kupandishwa kikosi cha kwanza mwaka 2012 na tangu mwaka 2013 amekuwa mchezaji muhimu wa kikosi cha kwanza cha Wekundu hao wa Msimbazi. 

No comments:

Post a Comment